WATU 18 wamefariki dunia, wakiwemo polisi wanne na viongozi wote wa kijiji
katika ajali mbaya iliyotokea Kijiji cha Utaho, Kata ya Puma wilayani Ikungi,
Mkoa wa Singida, ikilihusisha basi lenye namba za usajili T 799 BET aina ya
Nissan mali ya Kampuni ya Sumry.
Ajali hiyo ilitokea juzi usiku saa 2.45 katika barabara kuu ya Singida-
Dodoma umbali wa kilomita 15 kutoka Singida Mjini wakati basi hilo likitokea
mkoani Kigoma kwenda jijini Dar es Salaam.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Geofrey Kamwela, alisema kuwa ajali hiyo
ilitokea wakati wananchi na askari polisi wa doria walipokuwa wamekusanyika
kando ya barabara hiyo, wakijiandaa kuupakia mwili wa mwendesha baiskeli
aliyegongwa na lori katika eneo hilo na kufariki dunia.
Alisema kuwa askari hao walikuwa wakifanya kazi hiyo wakiwa ndani ya gari
lao lenye namba za usajili PT 1424 lililokuwa limeegeshwa kando ya barabara.
Kamanda alifafanua kuwa ghafla basi hilo liliwagonga watembea kwa miguu na
kusababisha vifo vya watu 15 papo hapo huku wengine watatu wakifariki dunia
wakati wakipatiwa matibabu.
Alisema kuwa dereva wa basi hilo, Paul Njilo mkazi wa Dar es Salaam,
alipokaribia eneo walipokuwa askari, aliligonga gari lao na katika kukwepa
aliwagonga wananchi pamoja na askari.
Kwa mujibu wa Kamanda Kamwela, dereva huyo hakusimama bali aliendelea na
safari kisha akalitelekeza basi hilo eneo la Ikungi, zaidi ya kiliomita 25
kutoka eneo la tukio na kutokomea.
Aliwataja askari waliokufa kuwa ni F.849 D/CPL Boniface Magubika wa CID
Wilaya ya Singida, F.6837 Pc Jumanne Mwakihaba wa FFU Singida, G.7993 Pc,
Novatus Tarimo wa ofisi ya RCO na G.8948 Pc, Michael Mwakihaba wa FFU Singida.
Pia aliwataja wengine waliokufa kuwa ni Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Utaho,
Ramadhan Mjengi; Paul Hamis, Mwenyekiti wa Kijiji cha Utaho; Ernet Salanga,
Mwenyekiti Kitongoji cha Utaho; Said Rajab, Usirika Itambu, Chima Mughenyi,
Salim Juma, Abeid Ramadhan, Mwinyi Hamis na Issa Hussein wote wakazi wa Kijiji
cha Utaho.
Kamanda Kamwela alisema miili ya marehemu wengine wanne bado haijatambuliwa
na ndugu zao na huku taratibu za kitabibu zikiendelea, na kwamba imehifadhiwa
katika Hospitali ya Mkoa wa Singida.
Alisema kuwa majeruhi wawili wamelazwa katika hospitali hiyo ya mkoa na
wengine sita katika hospitali ya misheni ya Malkia wa Ulimwengu, Puma.
Miili ya askari polisi inatarajiwa kusafirishwa kwenda mikoani wanakotoka
wakati wowote mara taratibu za kipolisi zikikamilika, ikiwa ni pamoja na kuwasiliana
na ndugu zao wa Rombo, Pwani, Mbeya na Iringa.
Akizungumzia kuhusu ajali hiyo, Kamanda Kamwela alisema awali saa 1:30 usiku
ilitokea ajali ya mtembea kwa miguu, Gerad Zefania aliyegongwa na lori na kufa
papo hapo.
Alisema kuwa upelelezi zaidi wa ajali hiyo unaendelea ili kujua chanzo
halisi cha tukio pamoja na kumtafuta dereva wa basi.
Katika hatua nyingine, watua wanaosadikiwa kuwa majambazi wakiwa wa silaha,
wamemuua kwa kumpiga risasi askari polisi mkoani Tabora na kumjeruhi mwingine
mmoja.
Tukio hilo lilitokea juzi saa 2:00 usiku katika Kijiji cha Usoke, Kata ya
Usoke, Wilaya ya Urambo.
Taarifa ya kuuawa kwa askari huyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na
Kamishina wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi, Paul Chagonja wakati
akizungumza na waandishi wa habari.
Chagonja alisema kuwa askari hao walikuwa wakielekea katika eneo la tukio
baada ya kupata taarifa ya kufanyika ujambazi eneo la Usoke.
Alisema kuwa askari hao wakiwa njiani walishambuliwa na majambazi hao
wanaodaiwa kufanya tukio la uporaji wa kutumia silaha kabla ya kumuua askari
huyo na kumjeruhi mwingine.Tanzania Daima
No comments:
Post a Comment