Pages

Tuesday, April 29, 2014

MAKUBWA ETI MENEJA BARCLAYS ALIPANGA WIZI

MENEJA wa Benki ya  Barclays Tawi la Kinondoni,  Alune Kasililika (28), anadaiwa kuchonga mpango wa majambazi kuvamia na kisha kupora kiasi kikubwa cha fedha katika  tawi hilo.


Katika tukio hilo lililotikisa Jiji la Dar es Salaam kwa takriban wiki tatu zilizopita, majambazi hao kwa kushirikiana na meneja huyo, wanadaiwa kuchota sh milioni 390. 2, dola za Marekani 5,5000, euro 2,150 na paundi 50.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Kamishna wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, alisema meneja huyo mkazi wa Kimara, alikula njama na baadhi ya  maofisa wake, majambazi ambao kwa pamoja walifanikisha kupora fedha hizo.

Alisema kuwa Meneja Kasililika, msichana mwenye umri wa miaka 28, alihamisha robo tatu ya fedha zilizoporwa siku moja kabla ya tukio na kumkabidhi mumewe ambaye hadi sasa ametolokea nje ya nchi na siku ya tukio la ujambazi ilikuwa sawa na kukamilisha sinema.

“Siku   ya tukio ilikuwa kama sinema. Ilikuwa ni siku ya kutekeleza uporaji huo kwani fedha nyingi zilichotwa siku moja kabla ya tukio na sinema hiyo ilichorwa na meneja huyo,” alisema Kamanda Kova.
Kova alisema uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa meneja huyo kwa kushirikiana na mfanyakazi mwenzake ambaye ni Operesheni Meneja wa tawi hilo,  Neema Bachu, walikula njama na watu wengine wa nje kufanikisha wizi huo.

Alisema uchunguzi huo pia unaonyesha kuwa meneja huyo na watu wake walikuwa na vikao mbalimbali vya maandalizi ya kufanikisha tukio hilo.
Mbali na meneja huyo na ofisa wake, wengine ambao wanashikiliwa na Polisi ni Frederick Lazaro (19), Kakamiye Julius (31) Idd Hamis (32), Sezary Masawe na Boniface Muumba (29).

Watuhumiwa wengine ambao walipohojiwa walikiri kuhusika na kukutwa na kiasi cha fedha ni Erasmus Mroto (38), Deo Olomy (32), Mohamed Athuman (31), Joseph Mkoi (33), Lucy Amos (30) na Grace Amon (39).

Wizi huo ulitokea  Aprili 15 mwaka huu majira ya saa tatu asubuhi katika tawi la benki hiyo baada ya majambazi hao kuwaweka chini ya  ulinzi watumishi wa benki hiyo na kupora fedha hizo.
Baada ya kupora fedha hizo, walikimbia kwa magari mawili, moja aina ya OPA lenye namba za usajili T 421 BQV rangi ya fedha, ambalo pia limekamatwa.

Wakati upelelezi wa tukio hili ukiendelea, polisi imewataka wananchi  waisaidie kwa kutoa taarifa ili kufanikisha kuwakamata waliohusika.Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment